Sudani: Waziri Mkuu mpya Abdalla Hamdok kuthibitishwa Agosti 20
Waziri Mkuu mpya nchini Sudani atatangazwa hivi karibuni. Jina lake limepitishwa Alhamisi, Agosti 15 na wawakilishi wa waandamanaji ambao walitakiwa kutoa jina la mtu atakayeshikilia nafasi hiyo.
Imechapishwa:
Waziri huyo mkuu mpya wa Sudan anaitwa Abdalla Hamdok na atathibitishwa Jumanne, Agosti 20 na Baraza Kuu la uongozi wa nchi, ambalo ni taasisi mpya la mpito.
Abdalla Hamdok, ambaye ni mchumi mbobezi alishikilia wadhifa wa naibu katibu wa Tume ya Uchumi ya Afrika katika Umoja wa Mataifa hadi mwaka jana.
Aliteuliwa bila kupingwa Alhamisi kuongoza serikali ya mpito ijayo nchini Sudani. Serikali ambayo raia watakuwa na nafasi muhimu kwani raia watapewa wizara 18. Jeshi litakuwa na wizara mbili tu, Ulinzi na Mambo ya Ndani.
Uchaguzi wa Abdalla Hamdok unatarajiwa kupitishwa rasmi Jumanne ya wiki ijayo. Uamuzi wa mwisho utatoka kwa Baraza Kuu, ambalo litaongoza katika kipindi chote cha mpito nchi hiyo.Taasisi hiyo inatarajiwa kuundwa Jumapili hii, Agosti 18, siku moja baada ya hafla ya kutiwa saini kwa makubaliano ya jumla yanayoweka masharti ya kipindi cha mpito na kugawana madaraka kati ya raia na jeshi.
Makubaliano hayo yalipatikana katika wiki za hivi karibuni baada ya miezi nane ya mvutano na machafuko ambayo yaligharimu maisha ya watu zaidi ya 250 upande wa waandamanaji. Makubaliano hayo pia yanatoa nafasi ya kuundwa kwa "Kamati ya Uchunguzi Huru" ili wahusika wa vitendo hivyo wawajibishwe.