Wagombea 26 kuwania kiti cha urais Tunisia
Wagombea ishirini na sita wamekubaliwa kuwania katika uchaguzi wa urais ujao nchini Tunisia, kati ya majina 97 yaliyowasilishwa.
Imechapishwa:
Miongoni mwa wagombea hao kuna wanaume 24 na wanawake wawili. Wagombea ambao hawakukubaliwa wana muda hadi Agosti 31 ili kukata rufaa.
Orodha ya wagombea hao imetangazwa na mamlaka inayohusika na uchaguzi, ISIE. Mamlaka hiyo imebaini kwamba wagombea hao 26 ndio wamekamilisha vigezo na masharti ya kuwania kiti cha urais.
Orodha hii haishangazi isipokuwa kukosekana kwa mgombea wa LGBT Mounir Baatour, ambaye maombi yake kuwania kwenye uchaguzi huo wa urais, yalikataliwa.
Kwa upande mwingine, majina yaliyotarajiwa yamekubaliwa, kama vile mwanzilishi wa kituo cha Televisheni cha Nessma TV, Nabil Karoui, Waziri Mkuu Youssef Chahed, naibu kiongozi wa chama cha Kiisilamu cha Ennahdha na Spika wa Bunge la Kitaifa Abdel Fatah Mourou, au Waziri wa Ulinzi, Abdelkarim Zbidi, mmoja kati ya wagombea wanaopewa nafasi kubwa ya kushinda uchaguzi ambaye anatwania kama mgombea binafsi.
Wagombea wengine hawakukamilisha vigezo na masharti ya kutosha. Ilikuwa inahitajika kuwa na saini za wapiga kura 10,000 sawa na saini kumi za wabunge, au saini 40 za mameya.