Rais wa zamani wa Sudan aonekana, kufunguliwa mashtaka
Rais wa zamani wa Sudan Omar Al Bashir ameonekana hadharani kwa mara ya kwanza, tangu alipoondolewa madarakani kutokana na shinikizo za wananchi mwezi April.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Bashir alionekana akiwa ndani ya gari la kijeshi akipelekwa katika Ofisi ya kiongozi wa Mashtaka kuhojiwa kwa tuhma za ufisadi.
Wiki iliyopita, Ofisi ya kiongozi wa mashtaka iliripoti kuwa itamfungulia mashtaka ya ufisadi, rais huyo wa zamani lakini pia anatuhumiwa kumiliki kiasi kikubwa cha fedha za kigeni kinyume cha sheria.
Bashir alionekana amevalia vazi la kitamaduni lenye rangi nyeupe, akitokea kwenye gereza maarufu la Kober jijini Khartoum ambako amekuwa akizuiliwa.
Wakati hayo yakijiri, raia wa nchi hiyo wanasubiri kuanza kwa mazungmzo kati ya uongozi wa kijeshi na wawakilishi wa waandamanaji, baada ya wiki iliyopita, pande hizi mbili kukubali kuja kwenye meza ya mazungumzo.
Watu 128 walipoteza maisha baada ya jeshi kuamua kusambaratisha maandamano ya raia wa nchi hiyo waliokuwa wamepiga kambi nje ya makao makuu ya jeshi, wakishinikiza jeshi likabidhi madaraka kwa raia.