Jean-Pierre Bemba kurejea nyumbani Juni 23
Makamu wa rais wa zamani wa nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Jean-Pierre Bemba ametangaza kuwa atarejea nchini mwake Juni 23, hatua ambayo inatajwa kuwa italeta wakati mgumu zaidi kwa rais Felix Tshisekedi.
Imechapishwa:
Bemba ambaye aliondolewa mashtaka ya uhalifu wa kivita na mahakama ya kimataifa ya ICC mwaka 2018 baada ya kutumikia kifungo cha miaka 11, ametoa tangazo hili kupitia ukurasa wake wa kijamii wa Twitter.
Kurejea kwa Bemba kutakamilisha orodha ya viongozi wa vuguvugu la Lamuka waliorejea nchini mwao akiwemo Moise Katumbi, Martin Fayulu, Adolphe Muzito, Antipas Mbusa Nyamwisi na Freddy Matungulu.
Bemba alikuwa miongoni mwa Makamu wanne wa rais wakati wa serikali ya mpito kati ya Julai 17 mwaka 2003 hadi Desemba mwaka 2006 na mwaka 2018 alikuwa miongoni mwa wanasiasa waliotaka kuwania urais nchini humo lakini baada ya majadiliano na wenzake, wakakubaliana kuwa Martin Fayulu awanie nafasi hiyo.
Mwaka 2006 aliwania urais na kumalizika katika nafasi ya pili, lakini mwaka 2007 alichaguliwa kuwa Seneta.