Mauaji yaripotiwa nchini Sudan baada ya jeshi kuvunja kambi ya waandamanaji
Watu watano wameuawa na wengine kujeruhiwa baada ya wanajeshi nchini Sudan kuamua kuvunja kambi ya waandamanaji jijini Khartoum siku ya Jumatatu.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kamati ya Madaktari wamethibitisha kutokea kwa mauaji hayo, baada ya wanajeshi kutumia nguvu kupita kiasi kwa kuwapiga risasi waandamanaji.
“Wote waliouawa wamepigwa risasi,” Kamati hiyo imesema kupitia ukurasa wake wa facebook.
Ubalozi wa Marekani jijini Khartoum, umelaani hatua hiyo na jeshi na kusema ni lazima ikome mara moja.
“Maafisa wa usalama wamevamia waandamanaji, hili ni kosa na lazima likome,” aliandika kupitia ukurasa wake wa Twitter.
Viongozi wa waaandamanaji wanasema kuwa wataendelea kupigania haki zao hadi pale jeshi litakapokabidhi madaraka, na wanasisitiza kuwa hata wakifukuzwa katika eneo hili watakwenda kupiga kambi katika eneo lingine.
Licha ya kukubaliana kuunda serikali ya mpito itakayodumu kwa muda wa miaka mitatu, pande zote mbili zimeshindwa kukubaliana kuhusu muundo wa serikali hiyo na ni nani atakayeingoza.
Haijafahamika ni lini mazungumzo hayo yatarejelewa ili kupata mwafaka.