Pata taarifa kuu
RWANDA-UGANDA

Rwanda, Uganda katika mzozo mwingine baada ya watu wawili kuuawa

Nchi za Uganda na Rwanda zimetupiana maneno baada ya Polisi wa Uganda kuwatuhumu wanajeshi wa Rwanda kuingia kwenye mpaka wa nchi yake na kutekeleza mauaji ya watu wawili, tukio ambalo limezidisha joto la mzozo baina ya nchi hizi mbili.

Waziri wa mambo ya nje wa Rwanda, Richard Sezibera hapa ilikuwa Machi 2019
Waziri wa mambo ya nje wa Rwanda, Richard Sezibera hapa ilikuwa Machi 2019 Cyril NDEGEYA / AFP
Matangazo ya kibiashara

Hata hivyo nchi ya Rwanda inakanusha vikali tuhuma za Uganda ikisema tukio hilo lilitokea kwenye mpaka wake baada ya maofisa wake kushambuliwa kwa mapanga.

Taarifa iliyotolewa na wizara ya mambo ya nje ya Uganda imesema kuwa “Serikali ya Uganda inakemea kwa nguvu zote ukiukwaji wa haki za kimipaka na wanajeshi wa Rwanda pamoja na uhalifu, vurugu na mauaji ya raia wasio na hatia”.

Uhusiano kati ya rais wa Rwanda Paul Kagame na mwenzake wa Uganda Yoweri Museveni ambao wakati fulani walikuwa washirika wakubwa, umeendelea kuzorota tangu mwanzoni mwa mwaka huu ambapo nchi hizi zinatuhumiana kwa makosa ya uhaini, mauaji ya kisiasa na kunguliana masuala ya ndani.

Taarifa ya jeshi la Polisi la Rwanda imesema kuwa, wanausalama wake walishambuliwa na watu waliokuwa na mapanga baada ya kusimamia pikipiki moja waliyohisi ilikuwa imeingiza vitu kimagendo ikitokea Uganda.

“Maofisa wetu waliwapiga watu wawili risasi, mmoja raia wa Rwanda ambae alikufa papohapo na raia mmoja wa Uganda ambaye nae alifariki baadae,” imesema taarifa hiyo ambayo imeongeza kuwa “Tukio hili limetokea Rwanda.”

Awali polisi ya Uganda ilisema tukio hilo lilitokea majira ya sambili usiku siku ya Ijumaa katika kituo cha mpaka kijijini Kiruhura kwenye wilaya ya Rukiga magharibi mwa nchi hiyo.

Nchi ya Rwanda imepunguza kwa kasi uagizaji wa bidhaa kutoka Uganda ambapo miezi michache iliyopita ilizuia raia wake kusafiri kwenda Uganda.

Hatua hii ya Rwanda ilijibiwa pia na Uganda ambayo nayo imekataza raia wake kutumia mpaka huo wa Rwanda.

Wataalamu wa wanaonya kuwa mzozo kati ya Rwanda na Uganda unatishia mustakabali wa ukuaji wa uchumi wa ukanda pamoja na utangamano hasa katika eneo ambalko kwa miongo kadhaa limeshuhudia baadhi ya nchi wanachama zikiwa kwenye vurugu za wenyewe kwa wenyewe.

Rais wa Uganda Yoweri Museveni amekiri kuwa amewahi kukutana na wapinzani wa rais Kagame lakini anakanusha kuwa hata mara moja amewahi kutangaza kuunga mkono harakati za uasi dhidi ya Serikali ya Rwanda.

Mzozo huu ulishika kasi mwezi Machi wakati Rwanda ilipotoka hadharani na kuituhumu Uganda kwa kuwateka raia wake na kuwaunga mkono waasi ambao wanataka kuipindua Serikali.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.