Waziri wa Mambo ya nje wa Ufaransa Jean Yves le Drian kuzuru DRC
Waziri wa mambo ya kigeni wa Ufaransa Jean Yves le Drian ambaye aliwahi kupinga ushindi wa DRC Felix Tshisekedi anatarajiwa jijini Kinshasa siku ya Jumatatu katika ziara ya kikazi.
Imechapishwa:
Akiwa jijini Kinshasa, le Drian anatarajiwa kukutana na kushauriana na rais Felix Tshisekedi ambaye amekuwa madarakani tangu mwezi Januari.
Ziara hii inakuja wakati huu kiongozi huyo wa DRC akiendeleza harakati za kidiplomasia kuomba uungwaji mkono kutoka kwa mataifa ya kigeni.
Tangu alipoingia madarakani, rais Tshisekedi, ametembelea mataifa karibu yote katika ukanda wa Maziwa Makuu lakini pia amewahi kwenda nchini Marekani.
Ufaransa ambayo inaisaidia DRC kutoa mafunzo ya polisi wake, na sekta ya afya miongoni mwa nyingine inapanga tena kumsaidia rais mpya wa nchi hiyo.
Ujio huu wa Jean-Yves Le Drian unalenga kudumisha uhusiano wa Kinshasa na Paris wakati huu nchi hiyo ikiendelea kukabiliwa na changamoto za kiusalama na ugonjwa wa Ebola Mashariki mwa nchi hiyo.