Upinzani waomba kusitishwa kwa mchakato wa uchaguzi
Baada ya uchaguzi wa wabunge kugubikwa na kasoro nyingi ikiwa ni pamoja na kususiwa na baadhi ya watu na wanasiasa nchini Benin, upinzani umemuomba rais wa nchi hiyo kusitisha mchakato wa uchaguzi.
Imechapishwa:
Upinzani huo uliowajumuisha wanasiasa mbalimbali wa upinzani ikiwa ni pamoja na marais wawili wa zamani Boni Yayi na Nicéphore Soglo, mke wake Rosine Soglo Vieira, aliyekuwa Waziri Candide Azannaï, mwakilishi wa USL, Sebastien Ajavon, ambaye anaishi uhamishoni nchini Ufaransa, na kiongozi wa Chama cha Kikomunisti.
Nicephore Soglo ndiye ambaye alisoma taarifa ya pamoja iliyotolewa na vyama kadhaa vya upinzani. Amesema wamefurahishwa na hatua ya wananchi wa Benin kususia kwa wingi uchaguzi wa wabunge. Upinzani umemuomba rais wa nchi hiyo kusitisha mchakato wa uchaguzi kabla ya leo Jumanne.
"Muda bado upo. Tuko tayari kusamehe. Anatakiwa aanzishe upya mazungumzo na wanasiasa wote ili kupata ufumbuzi muafaka kwa uchaguzi wa kidemokrasia na amani. Sio jambo la mchezo, " amesema Nicéphore Soglo.
Hayo yanajiri wakato maofisa wa tume ya uchaguzi wanaendelea kuhesabu kura ikiwa ni siku mbili tu zimepita tangu nchi hiyo ifanye uchaguzi wa wabunge ambao haukushirikisha mgombea hata mmoja wa upinzani.
Huduma ya mtandao iliyokuwa imesitishwa mwishoni mwa juma wakati wa uchaguzi, sasa imerejea.
Upinzani kwa upande wao wamekataa kutambua uchaguzi huo ambao umesema haukuwa huru na haki.
Hata hivyo Serikali kupitia kwa waziri wa mambo ya ndani, Sacca Lafia, amesisitiza kuwa uchaguzi wa mwishoni mwa juma lililopita ulikuwa huru na wa haki.