Umoja wa Afrika wataka jeshi la Sudan kukabidhi madaraka kwa raia
Baraza la amani na Usalama la Umoja wa Afrika, linataka jeshi nchini Sudan kukabidhi madaraka kwa raia kwa muda wa siku 15 zijazo, au nchi hiyo isimamishwe kuwa mwanachama wa Umoja huo.
Imechapishwa:
Wito huu wa Umoja wa Afrika, umekuja wakati huu waandamanaji wakiendelea kusalia nje ya makao makuu ya jeshi kushinikiza serikali nchini humo kuundwa na raia wa kawaida.
Jumatatu wiki hii Luteni Jenerali Jalal al-Deen al-Sheikh, mmoja wa viongozi wa kijeshi alikutana na Waziri Mkuu wa Ethiopia jijini Addis-Ababa na kusema kuwa, uongozi wa jeshi upo kwenye mchakato wa kumteua Waziri Mkuu, ambaye ataongoza serikali ya kiraia.
Wakati huo huo, kiongozi wa baraza la jeshi Abdel Fattah al-Burhan, ameendelea kupata shinikizo hizo baada ya kupokea simu kutoka kwa Mfalme wa Saudi Arabia, rais wa Falme za Kiarabu, Emir wa Qatar na rais wa Sudan Kusini.
Kansela wa Ujerumani Angela Merkel, naye akizungumza na rais wa Misri Abdel Fattah al-Sisi kwa njia ya simu, ametaka raia kukabidhiwa madaraka haraka iwezekanavyo.