Wakaazi wa Yumbi, Beni na Butembo kuwachagua wabunge
Serikali ya DRC imethibitisha kuwa Uchaguzi wa wabunge utaendelea kama ulivyopangwa siku ya Jumapili katika maeneo baada ya kuahirishwa kutoka mwisho wa mwezi Desemba mwaka 2018 kwa sababu za kiusalama na wasiwasi wa ugonjwa hatari wa Ebola.
Imechapishwa:
Uchaguzi huo utafanyika katika miji ya Butembo na Beni katika jimbo la Kivu Kaskazini pamoja na eneo la Yumbi katika mkoa wa Mai-Ndombe, Magharibi mwa nchi hiyo.
Tume ya Uchaguzi CENI imesema, imejiandaa vya kutosha kusimamia Uchaguzi huo na hakuna kitakachobadilika, na kila kitu kitaendelea kama ilivyopangwa.
Nayo, ofisi ya rais jijini Kinshasa, inasema usalama umeimarishwa katika maeneo hayo, kuhakikisha kuwa kila mmoja anapiga kura.
Viongozi wa maeneo hayo wametoa wito kwa wapiga kura kujitokeza kwa wingi kuwachagua wawakilishi wao.
Wabunge 15 wanatarajiwa kuchaguliwa katika Uchaguzi huo uliocheleweshwa.