Kumi na tano wauawa katika shambulio la bomu Mogadishu
Watu kumi na tano wameuawa katika shambulio la bomu lililotegwa katika gari ndogo karibu na hoteli na migahawa miwili mjini Mogadishu nchini Somalia. Wanawake watano ni miongoni mwa waliouawa, kwa mujibu wa polisi.
Imechapishwa:
"Idadi ya watu waliouawa kwa sasa ni kumi na tano ikiwa ni pamoja na wanawake watano, na 17 wamejeruhiwa," Abdikadir Abdirahman, mkurugenzi wa idara ya magari ya wagonjwa ameliambia shirika la habari la Reuters.
Hakuna kundi ambalo limedai kuhusika na shambulio hilo.
Hivi karibuni waasi wa kundi la wanamgambo wa Kiislamu la Al Shabab waliendesha shambulio lililolenga hoteli Wehliye ambayo imeshambuliwa leo Alhamisi. Hoteli hiyo inapatikana katika mtaa wa Maka al Moukaram, mtaa ambao ni maarufu sana kwa mji wa Mogadishu.
Siku ya Jumamosi wiki iliyopita, mashambulizi mawili na ufyatulianaji risasi viliua watu 15 katika mji mkuu wa Somalia, Mogadishu.