ACBF: Sera bora za uchumi zitabadili sura ya bara la Afrika
Wataalamu wa masuala ya fedha na uwezeshaji wanasema kuwa bara la Afrika linahitaji kwa kiwango kikubwa kuwa na sera zitakazolenga kuongeza uzalishaji kwenye sekta ya kilimo, ujenzi wa viwanda na ushawishi wa ufanyaji biashara kati ya nchi wananchama za umoja wa Afrika.
Imechapishwa:
Kwa mujibu wa mkurugenzi mtendaji wa taasisi ya mfuko wa kuzijengea uwezo nchi za Afrika, Profesa Emmanuel Nnadozie, anasema sera nzuri ambazo zinachochea uuzaji wa bidhaa nje, kuvutia uwekezaji na ujenzi wa miundombinu rafiki inayozingatia teknolojia ya kisasa ni suala linalopaswa kuwa kipaumbele kwa maendeleo ya bara la Afrika.
Profesa Nnadozie anasema kuwajengea uwezo vijana, kuwa na watu wenye ujuzi na wabunifu ni vichocheo chanya kwa ukuaji wa uchumi wa bara la Afrika.
Hata hivyo mbali na kueleza kuridhishwa na hatua ambazo Afrika imeanza kuchukua kutatua changamoto za kiuchumi, anaona bado baadhi ya viongozi wanakosa utashi wa kisiasa hasa katika kushughulikia changamoto za kikanda akitolea mfano mzozo kati ya nchi za Rwanda zilizoko kwenye jumuiya ya Afrika Mashariki.
“Kama viongozi hawako tayari kusonga mbele, basi hatuendi popote na linakuwa ni suala la kisiasa zaidi kuliko kuwa suala la kiuchumi. Kwa hivyo ningependa kuona viongozi wa ukanda wa Afrika Mashariki wanaelewa kuwa kuna suala la kupata na kupoteza! Na ndio suala la uongozi lilivyo! Kwa hivyo natoa wito kwa umoja wa Afrika kutumia nafasi yake kuzioatanisha pande zinazokinzana ili kutatua changamoto hizi”.
Kwa upande wake mkurugenzi mtendaji wa taasisi ya sekta binafsi nchini Tanzania, Godfrey Simbeye, akizungumza na idhaa hii kando na mkutano wa mawaziri wa fedha unaondelea mjini Yaounde, amesema ikiwa bara la Afrika linataka kufikia maendeleo endelevu na kuwa na uchumi wenye ushindani na mataifa mengine duniani ni lazima nchi zishirikiane na sekta binafsi.
Ameongeza kuwa kwa mazingira yaliyopo haoni nchi za Afrika zikiendelea ila kushirikisha sekta binafsi kwa kuzitengenezea mazingira rafiki ya kufanya biashara na uwekezaji.
Hivi leo magavana wa benki kuu kutoka nchi wanachama za umoja wa Afrika wamekutana na kujadiliana namna bora ya kuwa na mfumo wa pamoja wa kifedha ikiwemo uwezekano wa kuwa na shirikisho la kifedha la umoja wa Afrika.