DRC yasalia bila serikali 4 wiki baada ya Tshisekedi kutawazwa kama rais
Ni wiki nne sasa tangu kutawazwa kwa rais mpya nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo. Nchi hii mpaka sasa haijawa na serikali mpya. Mawaziri mbalimbali wa serikali iliyokuepo wameanza kujiuzulu mmoja baada ya mwengine.
Imechapishwa:
Bunge la taifa limekuwa limetoa nafasi kwa mawaziri hao hadi usiku wa manane kuamua kuendelea kuhudumu katika serikali au kushiriki katika bunge.
Hata hivyo wadadisi wanasema kuwa rais mpya wa DRC, Felix Tshisekedi Tshilombo, ameshindwa kuunda serikali kutokana na mgawanyiko unaoikumba jamii ya wanasiasa nchini humo.
Wakati huo huo Waziri Mkuu Bruno Tshibala hajajiuzulu kwenye nafasi yake wala kukabidhi barua ya kujiuzulu kwa serikali yake, jambo ambalo hata hivyo, aliombwa kufanya. Mawaziri mbalimbali na wabunge wamelazimika kila mmoja kujiuzulu kwenye nafasi zao.
Lakini kujiuzulu haimaanishi kuachia ngazi . "Huwezi kuachia ngazi kabla ya kukabidhiana madaraka na warithi wetu," amesema msemaji wa serikali inayomaliza muda wake, ambaye hata hivyo, amekumbusha kwamba yeye na mawaziri wenzake wanaendelea kuratibu shughuli ndogo ndogo za serikali.
Kwa upande wa uundwaji wa serikali, kazi kubwa iko mikononi mwa rais mpya Felix Tshisekedi, kwa vile ni rais ambaye anatakiwa kuteua waziri mkuu kutoka kambi ya walio wengi bungeni.
Wengi wameendelea kukosoa kuchelewa kutangazwa kwa serikali mpya.