Laurent Gbagbo na Ble Goude waendelea kusalia jela
Kitengo cha rufaa cha Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu ICC kimeagiza kuendelea kuzuiliwa jela kwa rais wa zamani wa cote d'Ivoire Laurent Gbagbo na waziri wake wa zamani Charles Blé Goudé.
Imechapishwa:
Kitengo cha rufaa cha Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu ICC kimechukuwa hatua hiyo kufuatia hatua ya mwendesha mashitaka wa ICC kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa majaji wa Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu kumfutia mashitaka Gbagbo na waziri wake wa zamani na kuamuru waachiliwe huru.
Fadi El Abdallah, msemaji wa ICC amesema uamuzi huu wa kitengo cha rufaa cha Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa kuendelea kumzuia Laurent Gbagbo na Charles Ble Goude umechukuliwa na majaji watatu kati ya watano.
Kitengo cha rufaa kimebaini kwamba kuna "sababu za kipekee" za kuendelea kumzuia jela Laurent Gbagbo na Charles Blé Goudé kwa kusubiri uamuzi kuhusu rufaa ya mwendesha mashitaka.
Mwendesha mashitaka ana hofu kuwa ikiwa Laurent gbagbo na charles Ble Gouge wataachiliwa huru itakuwa vigumu kuwapata ikiwa kesi yao itaendelea kusikilizwa miezi michache ijayo.
Kuzuiliwa kwao ni kwa muda, kitengo cha rufaa cha Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu kimesema.
Mwendesha mashitaka ana hadi Januari 23 kufikisha hoja zake kuhusu uamuzi wake wa kukata rufaa ya dhidi ya kuachiliwa huru kwa wawili hao.
Upande wa utetezi na walalamikaji wana hadi Januari 29 kutuma hoja zao zinazoeleweka.
Kesi hiyo imepangwa kusikilizwa Februari 1 katika kitengo cha rufaa.