UN yasikitishwa na vurugu za uchaguzi nchini DRC
Kampeni za Uchaguzi zinaendelea nchini DRC mwishoni mwa juma hili, huku wagombea wakiendelea kuwashawishi wapiga kura kuwaunga mkono siku ya kupiga kura tarehe 23 mwezi huu.
Imechapishwa:
Wakati kampeni zikiendelea Tume ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa, imelaani vikali kulengwa kwa wagombea urais kupitia vyama vya upinzani na wafuasi wao.
Mkuu wa Tume hiyo Michelle Bachelet, amesema anasikitishwa sana na mauaji yanayotokea hasa katika mikutano ya wagombea wa upinzani na hadi sasa watu sita wamepoteza maisha.
Mataifa ya Marekani, Canada, Uingereza na Uswizi kupitia mabalozi wao jijini Kinshasa, nao pia wameshtumu mauaji haya ya kisiasa.
Muungano wa nchi za Kusini kwa Afrika SADC, umetoa wito wa utulivu kipindi hiki cha kampeni.
Martin Fayulu, wiki hii akiwa mjini Goma, alisema anasumbuliwa na maafisa wa serikali wanaojaribu kumzuia kufika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo kutafuta kura.