Ebola: Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuzuru DRC Ijumaa
Wakati ugonjwa wa Ebola unaendelea kushika kasi katika maeneo ya mashariki ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa linasema linatiwa wasiwasi na kusambaa kwa ugonjwa huo nchini humo.
Imechapishwa:
Baraza la usalama pia limeonya kwamba homa hiyo inaweza kuenea katika taifa jirani la Uganda baada ya kugunduliwa kwa kesi kadhaa katika eneo la mpakani.
Kutokana na hali hiyo Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa linatarajia Ijumaa wiki hii kufanya ziara ya dharura kuelekea nchini DRC ili kutathmini matatizo ambayo wahudumu wa Umoja wa Mataifa wanakabiliwa nayo katika kutoa msaada katika maeneo yaliyoathirika.
Kwa mujibu wa vyanzo kutoka baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa mapigano makali nchini DRC yametatiza jitihada za kudhibiti kuzuka kwa virusi vya Ebola.
Mapigano makali kati ya makundi ya watu wenye silaha mashariki mwa Drc, hasa katika mji wa Beni yamewalenga raia na wahudumu wa afya wa Umoja wa Mataifa na kukwamisha jitihada za kuzuia kuenea kwa Ebola nchini DRC na majirani zake.
Kulingana na takwimu zilizotolewa na wizara ya afya nchini DRC ugonjwa huo umeua watu zaidi ya mia moja tangu Agosti 1 mwaka huu.