Ethiopia na Eritrea watia saini mkataba mpya wa amani
Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed na Rais wa Eritrea Isaias Afwerki siku ya Jumapili walisaini mkataba mpya wa amani wakati wa sherehe huko Jeddah, nchini Saudi Arabia.
Imechapishwa:
Julai 9 wawili hawa walitia saini "tamko la pamoja la amani na urafiki", na hivyo kufufua uhusiano wa nchi hizi mbili, miaka ishirini baada ya mgogoro wa kivita kati ya nchi hizo mbili (1998-2000).
Maelezo ya mkataba uliyotiliwa saini siku ya Jumapili na kutangazwa na serikali ya Saudi Arabia hayakufahamishwa. "Mkataba huu utasaidia kuimarisha usalama na utulivu katika eneo hilo," Waziri wa Mambo ya Nje wa Saudi Arabia Adel al-Djoubeir ameandika kwenye ukurasa wake wa Twitter Twitter, bila kutoa maelezo zaidi.
Sherehe hiyo ilihudhuriwa na Mfalme Salman wa Saudi Arabia, Mwanamfalme mkuu Mohammed bin Salman na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres.
Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) pia umesema kuwa umechangia katika kupatanisha Addis Ababa na Asmara. Abiy Ahmed na Isaias Afwerki walizuru nchi hiyo wiki chache baada ya kutia saini makubaliano ya kihistoria mwezi Julai ili kukutana pamoja na Sheikh Mohammed bin Zayed al Nahyan, Mfalme mtarajiwa wa Abu Dhabi.