OCHA: Mapigano mashariki mwa Libya yanatisha
Mapigano nchini Libya yameendelea kuongezeka mashariki mwa mji wa Derna, na kuzua hali ya wasiwasi nchini humo, kwa mujibu wa Ofisi ya shirika la Umoja wa Mataifa inayoratibu masuala ya kibinadamu na misaada.
Imechapishwa:
Mapigano katika mji wa mashariki wa Derna, nchini Libya yamefikia kiwango cha kipekee na mashambulizi ya anga, mashambulizi katika maeneo ya makazi na mapigano ya nchi kavu, Ofisi ya shirika la Umoja wa Mataifa inayoratibu masuala ya kibinadamu na misaada(OCHA) imesema Alhamisi wiki hii.
OCHA inaripoti uhaba mkubwa wa maji, chakula na huduma na upatikanaji wa maji safi na umeme umekatwa kwa wakazi takriban 125,000 wa mji wa Derna, unaozingirwa na wapiganaji wa kundi linalojiita Jeshi la Taifa la Libya ( ANL) tangu Julai 2017.
Libya imeendelea kukumbwa na mapigano ya wenyewe kwa wenyew, mapigano ambayo yamesababisha vifo vya mamia ya watu na wengine wengi kulazimika kuyahama makazi yao.
Libya imeendelea kukosa amani, huku wanajeshi wa serikali wakiendelea kupambana na makundi ya waasi tangu kuuawa kwa kiongozi wa nchi hiyo Muammar Gaddafi mwaka 2011.