Wananchi wa Misri wanapiga kura kuchagua rais katika uchaguzi tata
Wananchi wa Misri wanapiga kura Jumatatu ya wiki hii kuchagua rais kati ya rais wa sasa Abdel Fattah al-Sisi na mgombea mwingine mdogo ambaye anakabiliwa na ukosoaji mkubwa kuwa ni kibaraka wa Sisi
Imechapishwa:
Vituo vya kupigia kura vilifunguliwa majita ya 7 asubuhi katika zoezi litakalochukua siku tatu ambapo rais al-Sisi anatarajiwa kushinda kwa muhula wa pili wa kipindi cha miaka minne.
Usalama umeimarishwa nchi nzima kutokana na tishio la kutekelezwa mashambulizi na wapiganaji wa kiislamu wa Islamic State ambao wametishia kushambulia maeneo ya mitambo ya kupokelea matokeo na hata kwenye vituo.
Siku ya Jumamosi polisi wawili waliuawa katika shambulio la bomu kwa kutumia gari, shambulio likilenga msafara wa mkuu wa usalama kwenye jimbo la Alexandria.
Jumla ya wapiga kura milioni 60 wameandikishwa kupiga kura katika taifa ambalo asilimia kubwa raia wake ni waarabu.
Wananchi watapiga kura kuanzia Machi 26, 27 na 28 na matokeo rasmi yanatarajiwa kutangazwa April 2 mwaka huu.
Wapiga kura wanamachaguo mawili kati ya rais al-Sisi na Moussa Mostafa Moussa ambaye alijiandikisha siku moja kabla ya kufungwa kwa zoezi la kusajili wagombea wa nafasi ya urais na kuepusha uchaguzi kuwa wa mtu mmoja.
Moussa ambaye amekanusha kuwa kibaraka wa Sisi, alikuwa mstari wa mbele kumpigia kampeni achaguliwe kwa muhula wa pili hadi pale alipotangaza kuwa nae ni mmoja wa wagombea watakaochuana na al-Sisi.
Wagombea wengine waliwekwa kando akiwemo aliyewahi kuwa mkuu wa masuala ya utawala jeshini Sami Anan ambaye alizuiliwa mwezi Januari punde tu baada ya kutangaza kuwa atawania urais.
Jeshi lilidai kuwa Anan alivunja sheria kwa kutangaza kuwania urais kinyume cha sheria.
Akihojiwa kwenye kituo kimoja cha televisheni kuelekea uchaguzi huu Sisi alidai kuwa kukosekana kwa wagombea makini wa kushindana nae hakuhusika katika kuwafanya wasiteuliwe kuwania.
“Natamani tungekuwa na mmoja, au wawili, au watatu au wagombea 10 makini na ukachagua yukle unayemtaka,” alisema Sisi.
Sisi alishinda muhula wake wa kwanza katika uchaguzi wa mwaka 2014 mwaka mmoja baada ya mkuu huyo wa majeshi kumuondoa madarakani mtangulizi wake Mohamed Morsi kulikotokana na maandamano ya nchi nzima kushinikiza kujiuzulu kwake.