Pata taarifa kuu
FRANCOPHONE-TANZANIA

Clavier: Lugha bado ni kiungo muhimu cha tamaduni na umoja tuzilinde

Jumuiya ya Kimataifa ya nchi zinazozungumza lugha ya kifaransa “Francophone” zinasema lugha mbalimbali duniani zimeendelea kukabiliwa na changamoto na baadhi yao zimeanza kupotea na nyingine hazizungumzwi tena.

Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania, Frédéric Clavier akizungumza akiwa Dar es Salaam, 14 Machi 2018.
Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania, Frédéric Clavier akizungumza akiwa Dar es Salaam, 14 Machi 2018. Emmanuel Makundi/RFIKiswahili
Matangazo ya kibiashara

Wakizungumza jijini Dar es Salaam wakati uzinduzi wa wiki ya maadhimisho ya Francophone, mabalozi wa nchi 10 wanaowakilisha mataifa yao nchini Tanzania, wamekiri kuwa mabadiliko ya kiteknolojia na utandawazi yameathiri ukuaji na kuenea kwa baadhi ya lugha ikiwemo Kifaransa.

Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania Frédéric Clavier amesema “takwimu zinaonesha kuwa kidunia kuna lugha zaidi ya elfu 6 zinazozungumzwa na kila mwaka lugha zaidi ya 100 zinapotea kwa sababu hazizungumzwi tena au haziingiliani kitamaduni wala kibiashara”.

“Tunapaswa kuwa makini na kuzitunza lugha hizi, Jumuiya ya Francophone inahamisha matumizi ya lugha zikiwemo zile lugha mama kwa sababu tunaamini tunapaswa kuiepusha dunia na vita ya utandawazi” alisema Balozi Clavier.

Akijibu swali la mwandishi wa habari wa idhaa ya Kiswahili ya Radio France International ikiwa jumuiya hiyo inaridhishwa na uhamasishwaji wa lugha ya kifaransa kwenye nchi za Afrika Mashariki, Balozi Clavier amekiri jitihada zaidi zinahitajika kuhamasisha matumizi ya lugha ya Kifaransa kwa nchi wanachama.

Balozi wa Uswis nchini Tanzania Florence Mattli (kushoto), balozi wa Ufaransa Tanzania Frederic Clavier (katikati) na balozi msaidizi wa Canada Susan Steffan, 14 Machi 2018
Balozi wa Uswis nchini Tanzania Florence Mattli (kushoto), balozi wa Ufaransa Tanzania Frederic Clavier (katikati) na balozi msaidizi wa Canada Susan Steffan, 14 Machi 2018 Emmanuel Makundi/RFIKiswahili

Balozi Clavier amesema ni ukweli usiopingika kuwa kutokana na mabadiliko mbalimbali yanayoshuhudiwa hivi sasa duniani na kwa baadhi ya nchi kupitia mabadiliko ya kimfumo hasa katika kuamua matumizi ya lugha inayopaswa kutumika kitaifa, Jumuiya yao itaendelea kuwa mstari wa mbele kushirikiana na nchi zinazotumia lugha ya Kiingereza kuhimiza matumizi ya Kifaransa.

Amesema changamoto iliyopo kwa sasa kwenye nchi za ukanda wa Afrika Mashariki kuhusu matumizi ya lugha ya Kifaransa ni kuwa wananchi wengi wanapendelea kuzungumza kiingereza zaidi kutokana na utamaduni.

“Napenda nikiri kuwa tunahitaji kuongeza nguvu zaidi na tayari hatua kwa hatua tunaaminoi tutafikia mahali pazuri pengine kwa kuanza na kufanya tafsiri ya nyaraka mbalimbali kuwa katika lugha mbili za Kifaransa na Kiingereza” aliongeza Balozi Clavier.

Kwa mujibu wa takwimu zilizopo zinaonesha kuwa asilimia 50 ya watu wanaozungumza Lugha ya Kifaransa katika maisha yao ya kila siku ni watu kutoka barani Afrika.

Hivi leo kuna watu zaidi ya milioni 275 ambao ni Francophone duniani na inakadiriwa kuwa idadi hii itaongezeka kufikia watu milioni 700 ifikapo mwaka 2050.

Baadhi ya watu wanasema kuwa Kifaransa ni lugha ya Afrika na moja kati ya lugha rasmi zinazotumiwa kwenye umoja wa Mataifa.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.