Viongozi wa nchi zilizotuma majeshi Somalia wanakutana Uganda
Viongozi kutoka Mataifa ya Afrika, yaliyotuma wanajeshi wake nchini Somalia chini ya mwavuli wa umoja wa Afrika na kuunda kikosi cha AMISOM, kupambana na kundi la kigaidi la Al Shabab, wanakutana jijini Kampala kuthmini hali ya usalama katika taifa hilo na operesheni za jeshi hilo.
Imechapishwa:
Mkutano huu utaongozwa na rais Yoweri Museveni na kuhudhuriwa pia na viongozi wa Somalia.
Wakuu wa Majeshi kutoka mataifa yaliyotuma jeshi lake Somalia, na Mawaziri wa Mambo ya nje kutoka mataifa hayo walikutana kwa siku mbili zilizopita, na wanataka Jumiya ya Kimataifa kuongeza ufadhili zaidi wa kifedha ili kufanikisha vita dhidi ya Al Shabab na kuisaidia serikali dhaifu ya Somalia.
Kundi la Al Shabab linaendelea kuhatarisha usalama nchini Somalia, huku raia wakiendelea kuyatoroka makazi yao.
Nchi ambazo zilituma majeshi yao kusaidi serikali ya Somalia zimekua zikiomba kikosi hicho cha Umoja wa Afrika kisaidiwe kifedha na vifaa vya jeshi ili kulitokomeza kabisa kundi la Al Shabab.
Kundi la Al Shabab limeendelea na mashambulizi yake katika maeneo mbalimbali ya nchi ya Somalia, lakini vikosi vya usalama na ulinzi ndivyo vinalengwa hasa na mashambulizi hayo.
Mpaka sasa haijajulikana kundi hili linaendesha harakati zake kwa ufadhili kutoka nchi gani au makundi gani yanayolifadhili.