Gambia yarejea tena kwenye Jumuiya ya Madola
Nchi ya Gambia imerejea tena kwenye Umoja wa nchi za Jumuiya ya Madola, miaka mitano baada ya rais wa zamani Yahya Jammeh kuiondoa.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Jammeh ambaye aliondoka madarakani mwaka 2017, aliiondoa nchi hiyo baada ya kudai kuwa Jumuiya hiyo ilikuwa ya wakoloni.
Uanachama wa Gambia umekubaliwa tena katika Ofisi ya Jumuiya hiyo jijini London nchini Uingereza.
Baada ya kuingia madarakani, rais wa sasa Adama Barrow, aliahidi kuirejesha nchi hiyo kwenye Jumuiya hiyo katika harakati za kuimarisha uhusiano wa nchi yake na mataifa ya nje.
Gambia inakuwa nchi ya nne kurejea kwenye Jumuiya hiyo baada ya Afrika Kusini, Pakistan na Fiji katika miaka ya hivi karibuni.
Jumuiya ya nchi za Madola iliundwa mwaka 1931 kwa lengo la kuziunganisha nchi zinazozungumza lugha ya Kiingereza.
Inaundwa na mataifa 52.
Kiongozi wa Jumuiya hiyo ni Malkia wa Uingereza Bi.Elizabeth wa pili.