Upinzani nchini Misri wataka raia kususia Uchaguzi wa urais mwezi Machi
Wanasiasa wa upinzani nchini Misri wanataka wananchi nchini humo kususia Uchaguzi wa urais uliopangwa kufanyika mwezi Machi mwaka huu.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Wanasiasa hao wametoa wito huu, kutokana na mazingira magumu yaliyowekwa na serikali kuzuia mpinzani yeyote dhidi ya rais Abdel Fattah al-Sisi anayewania tena kuongoza kwa muhula wa pili.
Hadi sasa, mgombea pekee wa urais ni rais al-Sisi kuelekea Uchaguzi huo.
Jumanne ndio siku ya mwisho kwa wale wanaotaka kuwania urais kuwasilisha maombi yao kwa Tume ya Uchaguzi lakini inaovyoonekana hakuna atakayefanya hivyo mbali na rais al-Sisi .
Aliyekuwa Mkuu wa Majeshi Sami Anan anazuiwa na jeshi baada ya kukamatwa pindi tu alipotangaza kuwa atakuwania urais.
Jeshi linadai kuwa, hakufuata utaratibu wa kijeshi kabla ya kuamua kuwania urais nchini humo.
Ripoti zinasema kuwa, amezuiwa katika kambi ya jeshi baada ya kukamatwa.
Naye, Khaled Ali, mwanaharakati na wakili wa masuala ya haki za binadamu alijiondoa baada ya kusema kuwa, mazingira ya kisiasa hayakuwa mazuri kumruhusu kuwania.
Wachambuzi wa siasa wanasema, rais al-Sisi hataki upinzani wakati wa Uchaguzi Machi, ambao ametoa wito kwa raia wa nchi hiyo kujitokeza kwa wingi kupiga kura.