Kiongozi wa upinzani nchini Zambia akanusha mashtaka ya uhaini
Kiongozi wa upinzani nchini Zambia Hakainde Hichilema, amefikishwa Mahakamani jijini Lusaka, na kukanusha mashtaka ya uhaini.
Imechapishwa:
Hichilema ambaye amekuwa akizuiliwa kwa miezi kadhaa sasa, amefunguliwa mashtaka kwa kuzuia msafara wa rais Edgar Lungu.
Kesi yake imeratibiwa kuendelea siku ya Jumatano wiki hii.
Tangu mwezi Aprili alipozuiliwa, mwanasiasa huyo ameendelea kudai kuwa alishinda Uchaguzi wa mwaka uliopita na kusisitiza kuwa mashtaka dhidi yake ni ya kisiasa.
Zambia imeendelea kuwa katika wasiwasi wa kisiasa tangu kuzuiliwa kwa Hichilema, na kusababisha rais Lungu kutangaza hali ya hatari nchini humo kwa kile alichokisema ni kwa sababu za kiusalama.
Ikiwa atapatikana na kosa, kiongozi huyo wa upinzani atahukumiwa jela miaka 15 au hata kuhukumiwa kifo.
Rais Lungu amekanusha madai ya kumlenga kisiasa Hichilema.
Upinzani umeendelea kushinikiza kuachiliwa huru kwa kiongozi wao, wito ambao pia umekuwa ukitolewa na viongozi wa Kanisa Katoliki nchini humo.