Watalaam wawili wa Umoja wa Mataifa wauawa nchini DRC
Mauaji yanaendelea kuripotiwa katika jimbo la Kasai katikati mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ambako miili ya wataalamu wawili wa Umoja wa Mataifa imepatikana.
Imechapishwa:
Waatalamu hao waliokuwa wanafanya kazi za amani nchini humo Michael Sharp raia wa Marekani na Zaida Catalan raia wa Sweden, walitekwa katika ya mwezi Machi wakiwa pamoja na raia wane wa DRC.
Inaaminiwa kuwa watu hao wameuawa na waasi wa Kamwina Nsapu ambao wameendelea kuzua hali ya wasiwasi katika eneo hilo mwaka uliopita.
Msemaji wa serikali ya Kinshasa Lambert Mende amesema ishara zote zimeonesha wazi kuwa watalaam hao wameuawa mikononi mwa waasi hao.
Wakati uo huo, Umoja wa Mataifa, Muungano wa Africa, AU pamoja na Muungano wa Ulaya, EU wamelaani vikali ripoti za mauaji hayo na yale ya polisi 39 wa serikali yaliyotekelezwa na waasi hao juma lililopita.
Jumuiya hizo zimevitaka vikosi vya ulinzi na usalama nchini DRC kujizuia kutumia nguvu, na kuihimiza serikali kuendeleza mazungumzo na wanamgambo wa Kamuina Nsapu.