Rais Ian Khama amuomba Mugabe kujiuzulu
Rais wa Botswana Ian Khama akinukuliwa na shirika la habari la Reuters amemtaka mwenzake wa Zimbabwe Robert Mugabe kujiuzulu mara moja ili kuachia uongozi wa nchi kwa watu wengine kwa lengo la kuokoa uchumia wa taifa hilo ambao kwa sasa umefikia pabaya.
Imechapishwa:
Khama amemlaumu mweznake wa Zimbabwe kuwa hana uwezo tena wa kuinua uchumi wa nchi yake, na umri wake haumkubalii kukabiliana na hali hiyo. Amebaini kwamba kwa sasa nchi ya Zimbabwe inahitaji uongozi mpya ili kukabiliana na changaomoto za kisiasa na za kiuchumi zinazoendelea kulikwamisha taifa hilo.
''Umri wake na hali ambayo Zimbabwe ipo kwa sasa Rais Mugabe hana uwezo wa kutoa uongozi ambao unaweza kuinusuru nchi hiyo, " amesema Bw Khama.
Amesema raia wengi wa Zimbabwe wamelazimika kukimbilia ugenini kutokana na mgogoro uliopo nchini humo, huku baadhi wakielekea Botswana. Kwa sasa Botswana inawapa hifafhi zaidi ya raia 100,000 wa Zimbabwe.
Hata hivyo Rais Ian Khama, amewashtumu viongozi wanaotaka kusalia madarakani kwa muda mrefu, huku akibaini kwamba ataachia ngazi katika uongozi wa nchi ya Botswana mwaka 2018 baada ya kuhudumu kwa mihula miwili tu.
Itakumbukwa kwamba Rais Robert Mugabe ameliongoza taifa hilo tangu uhuru wake mwaka 1980 kutoka mikononi kwa Uingereza.