Mkutano wa IGAD unaendelea mjini Mogadishu huku usalama ukiimarishwa
Viongozi wa Mataifa ya Afrika Mashariki IGAD wanakutana mjini Mogadishu nchini Somalia, kujadili maswala mbalimbali yanayokumba mataifa hayo.
Imechapishwa:
Usalama umeimarishwa mjini Mogadishu huku viongozi kutoka Djibouti, Ethiopia, Kenya, Sudan Kusini, Sudan, Uganda na mwenyeji wao kutoka Somalia wakikutana kujadili maswala ya usalama na siasa nchini humo na Sudan Kusini.
Somalia inatarajiwa kuwa na uchaguzi wa wabunge mwezi huu, huku ule wa urais ukifanyika mwezi ujao katika zoezi linalolenga kuimarisha utawala wa Mogadishu.
Kabla ya kuanza kwa mkutano huu rais wa nchi hiyo Hassan Sheikh Mohamoud alisisitiza kuwa pamoja na kwamba kundi la Al Shabab limeondolewa mjini Mogadishu, usalama umeimarishwa kila kona ya mji huo.
Mara ya mwisho kwa Somalia kuwa mwenyeji wa mkutano mkubwa kama huu ilikuwa ni mwaka 1974, wakati ilipokuwa mwenyeji wa mkutano wa viongozi wa Afrika.
Wachambuzi wa maswala ya usalama wanasema hatua ya viongozi wa IGAD kukutana mjini Mogadishu ni kuonesha dunia kuwa vita dhidi ya Al Shabab vinazaa matunda na usalama unarejea nchini humo.