Burkina faso: RSP yapinga kupokonywa silaha
Juhudi za kukipokonya silaha kikosi cha ulinzi wa rais nchini Burkina Faso kilichorejesha mamlaka wiki iliopita baada ya kufanya mapinduzi zimegonga mwamba, kwa mujibu wa vyanzo vya kijeshi.
Imechapishwa:
Viongozi wa majeshi nchini Burkina Faso wanamlaumu jenerali Gilbert Diendéré kuwa ndiye anakwamisha zoezi hilo baada ya kuchukua uamzi wenye utata kuhusu hatua hiyo.
Kikosi cha walinzi wa rais kinaundwa na wanajeshi 1200. Hivi karibuni mkuu wa majeshi alikuwa amesema kuwa harakati ya kuwapokonya silaha wanajeshi wa kikosi cha ulinzi wa rais ilikuwa inaendelea vyema.
Viongozi wa Magharibi mwa Afrika waliafikia makubaliano ambayo yalitaka kikosi hicho kusalimu silaha zake na kurudisha mamlaka kwa serikali.
Rais wa mpito Michel Kafando alirudishwa madarakani Jumatano wiki iliyopita baada ya kundi linaloongozwa na jenerali Gilbert Diendéré kuwacha mamlaka na baadae kuomba msamaha raia na jumuiya ya kimataifa.